Friday, May 20, 2016

WAKIMATAIFA HAWA HAPA MWANANGU.

MASHUJAA walioitoa kimasomaso Tanzania kwa kufanikiwa kutinga hatua ya makundi ya michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, Yanga wanatua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Kambarage Nyerere, huku wakisema haikuwa kazi rahisi kuitoa Sagrada Esperanca ya Angola.
Yanga imesonga mbele baada ya ushindi wa jumla wa mabao 2-1, ikiwa ni kutokana na kushinda 2-0 katika mchezo wa kwanza jijini Dar es Salaam, kabla ya kukubali kipigo cha 1-0 ugenini juzi.
Katika mchezo huo wa juzi, wachezaji wa Yanga walikumbana na changamoto kadhaa kutoka kwa wapinzani wao, wakiwamo waamuzi walioonekana wazi kuwapendelea wenyeji hao.

Moja ya ‘figisu figisu’ hizo ni kitendo cha nahodha wake, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kuonyeshwa kadi nyekundu, mshambuliaji Donald Ngoma kuibiwa vitu vyake na kubwa zaidi ni mwamuzi kuwapa wenyeji penalti dakika za lala salama ambayo ilipanguliwa na kipa Deogratius Munishi ‘Dida’.
Kutokana na ushujaa ulioonyeshwa na Dida kwa kuokoa adhabu hiyo, mashabiki wa Sagrada walimpiga jiwe, lakini hilo hakikuwasaidia wenyeji hao kuhimili vishindo vya wakali wa Jangwani, maarufu kwa jina la Wakimataifa.
Kwa hali ilivyokuwa muda wote wa mchezo huo ikiwamo waandishi wa habari wa Tanzania kuzuiwa kupiga picha, ni wazi kuwa kupita kwa Yanga kwenye hatua hiyo ilikuwa ni zaidi ya vita kama alivyokiri kocha mkuu wa timu hiyo, Hans van der Pluijm, akiungwa mkono na baadhi ya wachezaji wake.
Akizungumza na BINGWA, Pluijm alisema haikua kazi rahisi kikosi chake kutinga hatua ya makundi kutokana na changamoto mbalimbali alizokutana nazo, huku akitamba kuwa na imani kubwa ya kufika fainali ya michuano hiyo.
Hata hivyo, Mholanzi huyo alisema kuwa hakushangazwa kikosi chake kutinga hatua ya makundi kwani analifahamu vyema soka la Afrika katika ngazi ya klabu.
“Sishangazwi na hatua hii tuliyofikia ya kuingia hatua ya makundi ya michuano ya Shirikisho, hii si mara yangu ya kwanza kuipeleka timu hatua hii, niliwahi kuifikisha hatua kama hii Berekum Chelsea (ya Ghana) mwaka 2012,” alisema Pluijm.
Alisema vijana wake walipambana na kujitoa muhanga katika mchezo huo wa juzi licha ya figisu figisu walizokutanazo kuhakikisha wanaipeperusha vyema Bendera ya Tanzania.
“Nawapongeza vijana wangu, japo tumefungwa bao 1-0, lakini cha muhimu tumefanikiwa kusonga mbele, ila ni vema tukafahamu bado tuna safari ndefu zaidi ya mafanikio,” alisisitiza.
Wakati huo huo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Yanga, Jerry Muro, amesema kuwa kikosi chao kinatua nchini leo saa 8:30 mchana wakitokea Angola na kwamba kitaenda moja kwa moja kambini kwa ajili ya safari ya kesho kwenda mjini Songea tayari kwa mechi yao ya mwisho ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Majimaji ya huko.
Aliwataka mashabiki wa Yanga kujitokeza kwa wingi Uwanja wa Ndege kuwalaki mashujaa wao watakaotua kwa kutumia ndege ya Shirika la Afrika Kusini (South African Airways).
Baada ya kutua, mashabiki wataandamana kuisindikiza timu yao hadi makao makuu yao yaliyopo Mtaa wa Jangwani, huku wakitarajiwa kuuteka Mtaa za Msimbazi yalipo maskani ya watani wao wa jadi, Simba.
“Bada ya mchezo wetu wa Jumapili dhidi ya Majimaji, timu itarejea Dar es Salaam Jumatatu kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wetu wa fainali ya Kombe la Shirikisho Tanzania (FA) dhidi ya Azam FC Jumatano ya wiki ijayo,” alisema

No comments:

Post a Comment

KATUNI ZA MWAGITO HIZI HAPA MWANANGU.